Wanne Wafungua Pazia la Fomu za Urais CCM

Pazia la Chama cha Mapinduzi (CCM) kupata mgombea wake wa urais katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba limefunguliwa rasmi jana mjini Dodoma.
Makada wanne walichukua fomu za kuwania nafasi hiyo, huku wakisindikizwa na wapambe wao na kukutana na Katibu wa Oganaizesheni, Dk Mohamed Seif Khatib aliyewakabidhi fomu hizo, katika ofisi za makao makuu ya chama hicho.
Shughuli hiyo ilitawaliwa na kila aina ya mbwembwe, shangwe na shamrashamra, hasa wakati wagombea hao walipokuwa wakizungumza na waandishi wa habari na kueleza mikakati yao ya kwenda Ikulu.
Waliochukua fomu jana ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira, Balozi wa Kudumu wa Umoja wa Afrika (AU), katika Umoja wa Mataifa (UN), Amina Salum na Mbunge wa Afrika Mashariki, Makongoro Nyerere.
Wakati makada hao wakitangulia, leo ni zamu ya wengine wakiwamo Makamu wa Rais Dk Mohamed Gharib Bilal na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, ambao tofauti na makada wengine, hawakuitisha mikutano ya kutangaza nia.
Kwa mujibu wa ratiba ya jana, mmoja kati ya waliotarajiwa kuchukua fomu alikuwa Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa lakini alishindwa ikielezwa kuwa alikuwa katika msiba wa Mbunge wa Ukonga, Eugen Mwaiposa.
Mbwembwe
Wagombea waliokuwa kivutio tangu katika uchukuaji wa fomu hadi kujibu maswali ya wanahabari ni Makongoro na Wasira, huku Profesa Mwandosya akiwaponda wagombea urais wanaojikita kuwaponda wenzao, badala ya kueleza watalifanyia nini Taifa. Mgombea wa kwanza kufika katika ofisi hizo akiwa na msafara wa magari manne na wapambe takriban 100 alikuwa Profesa Mwan dosya. Aliambatana na wabunge, Profesa David Mwakyusa (Rungwe Magharibi), Abdul Marombwa (Kibiti), Aliko Kibona (Ileje), Hilda Ngoye (Viti maalumu) na Mchungaji Lackson Mwanjali (Mbeya Vijijini).
Baadaye alifuatia Wasira, kisha Amina ambaye aliambatana na Mbunge wa Viti maalumu, Anna Abdallah huku Makongoro akifunga pazia la uchukuaji huo wa fomu jana.
Wasira na Profesa Mwandosya waliambatana na wake zao, huku Makongoro na Amina wakiwa na wapambe tu.
Dk Bilal na Dk Magufuli


Uchukuaji wa fomu unaendelea tena leo kuanzia saa nne asubuhi hadi saa 12 jioni na miongoni wanaotarajiwa ni Dk Bilal, Dk Magufuli, Amos Siyatenzi, Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye, Balozi Ali Karume na Lowassa.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment