Sehemu ya 4: ***KIMINI CHA MTOTO WA ASKOFU***

ILIPOISHIA Sehemu ya 3…..
Akaniambia "Chavala! Kazi ni nzuri sana, Hongera! Nakufuatilia sana, ila samahani, kuna wakati huwa majaribu yanatusonga kwa upesi ila Nakuahidi nitajirekebisha! Mmh! Jamani mbona sijakuelewa kwani kimetokea nini? Nikamuuliza, Akasema Chavala watu huwa wanakosea,hata mimi huwa nakosea, nikamtolea macho!
Akawa kama anashindwa kuongea na kushindwa kujiamini...Lakini kwa kujikaza akasema Chavala mimi ni.......

ENDELEA...

Sherehe ile iliendelea vizuri, keki ikakatwa na maharusi wakalishana kwa staili walioichagua wenyewe na watu wakagoganisha maglasi kwa furaha, wageni waalikwa wakacheza sana pamoja na maharusi na hatimaye ikafika saa ya kusikia Maneno ya Hekima toka kwa wazazi wa pande zote mbili na hapo ndio niligundua yalikuwepo mashindano na majivuno kwa hiyo sherehe, alianza Baba mkubwa wa Bwana harusi na akasema yafuatayo ninayoyakumbuka;

Mwanangu sasa umekua, umecheza sana imetosha, umeruruka imetosha na nafurahi ukaamua kuanza kusali, Hongera sana na huko Mungu amekupatia zawadi ya mke, (Vikasikika vigelegele) Najua Mungu hana upendeleo, kama ni yeye amekupa mke huyo ninaamini utayafurahia maisha yako, Ninaamini hautamwacha Mungu baada ya kufikia hapo, Sisi kama familia tutakuzawadia gari ya kutembelea lakini wakati wa sherehe yenu ya kutimiza mwaka mmoja wa ndoa! (Nilifikiri ni masihara au mbwembwe) basi nikapanga kumuuliza akimaliza, lakini mara nikamsikia mtu mmoja akisema “Huyu mzee anawapenda sana watoto wake na nasikia ana hela zake, sema watoto wake wengi wasumbufu, ila huyu ndio ameonyesha njia kwa kwenda kanisani na kufunga ndoa rasmi, na si umemsikia ameahidi gari, wala hatanii, amewema atawapa baada ya mwaka mmoja maana inawezekana haamini kama kwasasa litawafaa” basi hapo nikaelewa, nikaendelea kulitafakari na kulimezea tu.

Aliendelea….Mchungaji kanisani amewahubiria vizuri usiache kuyashika hayo, ndoa ni kama mtihani na kufaulu kwake kunategemea na umakini wako mwenyewe hivyo mkawe makini kwenye ndoa yenu....Nimalizie kwa maneno ya Mc Chavala aliyosema wakati fulani hapa kuwa....Kuwa alisoma shule msingi akapewa cheti alipohitimu, akaingia sekondari na pia akapata cheti alipohitimu na hata chuo kikuu pia alipata cheti chake mwishoni baada ya kuhitimu lakini cheti cha Ndoa alipewa wakati ndio anaanza maisha ya ndoa,maana yake hata aliyetoa cheti hawezi kusema wala kutabiri maisha yaliyo mbele...hivyo najua na ninyi ndio mmpewa cheti cha ndoa leo hivyo kufaulu ama kufeli kwenu kunategemea na ninyi, Mungu awabariki na tuwatakie maisha mema, Ahsante sana Mc!
(Akanirudishia kisemeo na kurudi kwenye kiti chake)

Yakapigwa makofi hapo na nikawapa wimbo mmoja wa asili yao na hapo wakacheza kwa raha zao na hapo ikafuata nafasi ya upande wa kike kutoa maneno ya hekima, ingawa mengi walishayasema wakati wa kumuaga binti yao huko kwao, basi nilipokaribisha mtu kutoka upande ule wa binti aliinuka Mama yake mzazi na Bibi harusi, nilimtambua kwasababu niliona alivyotambulishwa hapo kwanza na hapo nikaona kama watu kadhaa wakiinama chini kwa minong'ono, sikueelewa haraka, kuwa hakupangwa kuongea yeye ama sio mzuri kwenye kuongea ama lah! basi nikampatia nafasi ili aseme hekima zake kwa maharusi;

Na hapo mimi nikarudi nyuma, nikajipa nafasi kuanza kutafakari maneno ya yule mtumishi, yaani yule Mtume aliyeniambia kuwa yeye ameitwa kwa ajili utumishi mgumu, kwahiyo huwa anakwenda sehemu walizo wanawake wanaojiuza na hapo akimwona mmoja ambaye amekusudiwa siku hiyo, basi huenda naye kwenye nyumba za wageni na huko kwasababu ya Utulivu hukubali kumlipa kahaba huyo na kuanza kumhubiria habari njema za Mungu na kumshawishi aachane na biashara hiyo, na ndio maana siku ile nilimwona pale akiwa anaondoka! (Hayo maneno yalikuwa yake kwangu)

Kichwani mwangu maswali yamekuwa mengi kuliko majibu, Najiuliza hivi ana mke au watoto? Je kanisa lake linaitwaje? Na Je waumini kanisani wanajua utumishi wa Mtume wao? Je kuna waumini wangapi huko waliopatikana kwa huduma hiyo? Basi nikiwa nafikiria kuwa itabidi sasa hivi au wakati wa chakula nikakae nae mezani angalau nijue zaidi mawili matatu, nikajikuta navutwa usikivu na hekima za mama mzazi wa bibi harusi, Nazo zilikuwa njema ila za kutisha pia,Mimi nimesherehesha harusi nyingi na nimekumbana na vimbwanga kadhaa ila wakati huu nilijikuta hata mimi mgeni sana mitaa hii!

Mama alianza kwa maneno ya shangwe utasema yeye ni Mc pia,lakini wa sherehe za uswahilini labda; Na hapo akamfagilia yule Mtume kuwa mambo yake safi na hivyo akawataka hawa maharusi wasiache kutaka ushauri na maombi kwake,na kwa maneno yale na mengineyo nikajua kuwa yule mtumishi alikuwa mdogo wake kabisa.

Maneno ya mama yule yalikuwa mengi sana ila haya ni machache tu yaliyobaki vichwani mwa watu wengi, nikiwepo na mimi hata leo;

Mama alisema “Binti yetu tumekulea, tumekutunza na tumekusomesha ili uwe na maisha mazuri,tena Baba amekusomesha nje ya nchi hivyo najua huna ulimbukeni wa mambo kama watu wengine, mkwe wetu usichoke wala usimzuie mkeo anapotaka kusafiri kwenda nje maana unajua amezoea na hata akitaka kusoma zaidi mruhusu akasome tu maana akisoma ndio mafanikio yenu. Mwanangu usikubali kabisa kunyanyasika maisha ya manyanyaso yalipitwa na wakati. Mwanangu nataka ukaishi na mume wako vizuri, mkapendane sana, mkapate watoto mapacha na mapacha. Hatutaki mtoto wetu azeeke mapema hivyo tumekununulia mashine kufulia, tumekutafutia mpishi aliyesomea tutamlipa sisi, na tumewatafutia kitanda, Tv mbili kubwa ya chumbani na sebuleni, sofa ,makabati ya vyombo na nguo,jokofu Mama samahani sasa hivi ni maneno ya hekima tu zawadi ni baadae(Nilidakia kama Mc)

Mc wala usijali na mimi wala aikabidhi zawadi sasa hivi ila nataka tu Bwana harusi ajue binti yetu hana shida kihivyo, tumegharimia harusi hii ili iwe nzuri sana na pamoja kuwa maisha ya bwana harusi ni ya kawaida sana, bado tulimruhusu binti yetu aolewe na kijana maana ni chaguo lake! Kuhusu nyumba mkwe wangu usipate shida ipo, gari binti yangu lipo na tumwekuwekea kwenye Akaunti yako Milioni 50 kwa ajili ya kuwasaidia kama akiba mnapoanza maisha na mume wako...ila mkwe usije ukabweteka ukaacha kutafuta hela hata kama ni hizo hizo za kubangaiza ukifikiri vitu vyote ni kwa ajili yako hapana...Mwanaume majukumu!

Hapo sikusikia makofi wala vigelegele, ila ndugu wa Bwana harusi wamekasirika kama mbogo na wale wa bibi harusi wengi wameinamisha vichwa vyao chini, na yeye mama anaendelea kujimwaga tu....nikiangalia pale mbele niliona sura ya Bwanaharusi inabadilika taratibu na hapo akili ya haraka ikanijia nikamfuata Mhazini wa kamati ya maandalizi haraka ili animalizie pesa yangu ile nusu iliyobaki....Unajua ilipasa anipatie tu mara ile walipofika ukumbini lakini kwakuwa niliwaamini sikufanya haraka, na nilivyomfuata kwa bahati mzuri alikuwa nayo mfukoni, hivyo akanipatia bahasha yangu hapo, nikafungua tu kuchungulia, "Chavala Milioni moja hiyo!" Alisema kwa tabasamu, nikamwambia ngoja nitahesabu nikitulia na Ole wako ziwe pungufu hata elfu kumi tu utalipa faini, basi nikawa nakimbia mbele kuchukua kisemeo maana yule mama asingemaliza maneno yake, kama nisingesogea pale mbele

.....Huo ni ukweli na hayo ndio nilitaka niseme ili kila mmoja ajue kuwa tumemtunza binti yetu, tumemsomesha, tunampenda na tumefanya kila tuwezalo kuhakikisha haendi kuteseka, kutaabika, kunyanyasika wala kwenda kuishi maisha ya tabu huko aendako, tunawatakia maisha mema ua ndoa....Akanipa kisemeo na wakati anakwenda kukaa hakuna alipiga makofi wala kigelele ila misunyo na minong'ono na hapo kabla sijakaa vizuri, nilishtuka kuona Bwana harusi ananyanyuka kwa hasira na kuja kwangu! (Sio jambo la kawaida hilo, hivyo kila mtu alikuwa amehamaki kuona kinachoenda kutokea, najua hata wageni waalikwa pia walitibuka na maneno ya majivuno ya mama yule)

Alininyang'anya kisemeo huku machozi yakimtoka na akaanza akasema hasira na uchungu "Niliamua kumwoa mtoto wenu kwasababu niliamini anafaa kuwa mke wangu, pamoja na ugumu wa mchakato na manyanyaso wakati naleta mahari, niliamini ni ugumu ulionipasa kupitia ili kupata mke bora, lakini maneno haya ya mama yameonyesha majivuno kupita kiasi, majigambo na dharau na kwakuwa ninyi mnajiona mna kila kitu kwa ajili ya mwanenu basi nafikiri mimi sio mume wake sahihi, I am sorry baby! (Aliomba msamaha kwa mke wake huku akiwa na jazba yenye hasira na baada ya hapo akatoka ukumbini)

Ukumbi wote ukatahayaruki, wengine wanalia, wengine wanasikitika, Bibi harusi akawa anatoka kumkimbilia pamoja na wale wapambe, Wazazi wa Bwana harusi nao wakawa wanatoka nje na huku upande wa Bibi harusi nikaona kama mzozo, wengi wakimlalamikia mama mtu kwa maneno yake yale!

Kisemeo ninacho mkononi,sijui niseme nini,Dj wangu ananishangaa pia,wahudumu nao kila mmoja ana lake, na wageni waalikwa wengine wakawa wanaendelea kunywa juice zao mezani na pombe walizoingia nazo kimaficho huku wakijadili kadhia hiyo na ukweli kila mmoja alikereka, maana sio kwamba familia ya Bwana harusi walikuwa masikini kiasi cha maneno yote yale, ni kweli familia ya bii harusi ni matajiri sana tu ila ndio wameshaharibu sasa. Watu wengine wakawa wanaelekea nje ya ukumbi kuangalia hatma zao za kuelekea makwao!

Na ilikuwa ni tu baada ya Maneno hayo ya hekima twende tukapate Chakula cha siku ile maalum!
Wengine waliwaendea ndugu kufariji, wengine walisema bora imekuwa hivyo,wengine walisema walijua tu,wengine walibaki walikilia na kuomba na wengine walikuwa wakiondoka kimyakimya, basi na mimi nikaona ni vema nimwendee Bwana harusi, yamkini kuna jambo ningeweza kumshauri, Basi nikiwa naenda nje kwa kasi, nilitoka nje na kuanza kuangalia huku na kule sikuwa na muona, basi ikanibidi niende kuangalia kwenye eneo la maegesho ya magari kama gari yao bado ipo yamkini akawa huko, basi kwenye kona hivi niliteleza na kuanguka.

 Sikuumia sana maana nilijidaka kwenye ukuta mpaka kukaa chini, Sasa nilihisi chini kuna kama majimaji hivi maana niliteleza na mkono mmoja ulilowa maana ulitua chini, Sasa nikawa ninajiuliza haya maji yametoka wapi na hii ni njia tu, Nilipochukia simu yangu na kuwasha kurunzi na kumulika, nikagundua yale hayakuwa maji bali ni ilikuwa ni Damu, nilishtuka sana na kujaribu kumulika pande zote pale nilipokuwa na hapo nikaona damu imetapakaa mahali pakubwa, pale chini ilijaa na hata mimi nilikuwa nimekaa juu ya damu.......ITENDELEA!

(c)King Chavvah, 2015
+255 713 883 797
Instagram: kingchavvah
Twitter @kingchavala


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment