CCM Inamhitaji Lowassa Ili Ishinde Uchaguzi- Kingunge

Mwanasiasa mkongwe nchini, Kingunge Ngombale-Mwiru amesema CCM inamuhitaji Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kwenye mchakato wa Uchaguzi Mkuu na kukitaka chama hicho kujadili jambo hilo ili kuondoa tofauti zilizojitokeza kabla ya kupiga kura za kumchagua Rais na wabunge.
Katibu huyo wa zamani wa halmashauri Kuu ya CCM amesema Kamati ya Maadili na Usalama iliteka majukumu ya Kamati Kuu baada ya kuamua kuchuja majina ya makada waliojitokeza kuwania urais kwa tiketi ya chama hadi kufikia watano, akisema jitihada hizo zilizofanywa kuvunja kanuni zililenga kumuengua Lowassa kuwania kuingia Ikulu.
Akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake jijini Dar es Salaam jana, Kingunge, ambaye alijitokeza waziwazi kumpigia debe Lowassa, alisema kitendo cha kumuengua Lowassa kwa kuvunja kanuni kimeacha kasoro kubwa ndani ya chama hicho tawala kwa sababu taratibu zilikiukwa ili kupata viongozi.
Alisema kosa hilo si la Dk John Magufuli aliyepitishwa kuwa mgombea urais wa CCM, na wala si la Lowassa, bali ni la waliopendekeza majina ya walioingia tano bora.
Jina la Lowassa, ambaye alijidhihirisha kukubalika ndani na nje ya CCM kutokana na harakati zake za kusaka wadhamini kujaa watu, halikupelekwa kwenye Kamati Kuu, kwa mujibu wa Kingunge na hivyo kutojadiliwa na chombo hicho ambacho kilimpitisha Dk Magufuli, Dk Asha Rose Migiro, January Makamba, Bernard Membe na Balozi Amina Salum Ali.
“Jitihada zote ambazo zimefanywa za kuvunja taratibu zilikuwa zinaelekezwa kwenye kumzuia Lowassa asipate haki. Badala ya yote nani kashinda? Kashinda Lowassa kwa sababu imeonekana wazi kuwa yeye ndio kipenzi cha Watanzania na hakuna kitu kikubwa kama kupendwa na watu,” alisema.
“Kuanzia sasa wana-CCM tutafute namna ya kushikamana vizuri, tuimarishe umoja wetu maana ndio nguvu yetu na katika hili ndugu Lowassa ana nafasi muhimu na ya kimkakati ana mamilioni ya Watanzania wana imani naye. “Mpaka sasa tunaulizwa maswali kutoka pande zote za nchi, hatuna majibu. Tukitaka kufanikiwa kama chama tuunde mazingira yatakayotuwezesha kutumia nguvu tulizonazo twende katika uchaguzi na tushinde kwa kishindo. Lakini lazima yaliyotokea yazungumzwe ndani ya chama maana tunahitaji ushirikiano wa Lowassa.”
Akielezea utaratibu wa uteuzi wa wagombea, Kingunge alisema Halmashauri Kuu ya CCM ndiyo inachagua Kamati Kuu ya chama inayoitwa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa na ndiyo ambayo inaunda chombo cha Halamshauri Kuu ya Taifa kinachoitwa Kamati Kuu.
Alisema pia Halmashauri Kuu inaunda Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa, kwamba ndani ya CCM vipo vitengo ambavyo vinahudumia vikao, kikiwamo cha Kamati ya Maadili.
Alisema kwa utaratibu wa kikatiba, kazi ya sekretarieti ni kuhudumia Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa, katika kupitisha wagombea urais, Sekretarieti hukusanya majina ya walioomba kugombea na kuwasilisha taarifa yake kwenye Kamati Kuu.
“Sekretarieti si kikao cha maamuzi, wala si kikao rasmi cha mapendekezo. Mchakato hasa unatakiwa uanzie kwenye Kamati Kuu na ndiyo utaratibu uliotumika mwaka 1995. Wagombea wote wanatakiwa kupita Kamati Kuu na kila mmoja kujieleza sababu za kutaka kugombea urais,” alisema.
Katika kuteua mgombea urais wa CCM, vikao vya Kamati ya Maadili na Usalama, Kamati Kuu, Halmashauri Kuu na Mkutano Mkuu vilipishana kwa muda mfupi kutoka kikao kimoja hadi kingine na kufanya suala hilo liamuliwe katika muda wa siku mbili.
Crdt: Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment