Kizungumkuti CCM, JK Awataka Wagombea Wasinune

 Rais Jakaya Kikwete amesema idadi ya wanachama wa CCM waliojitokeza kuwania urais ni kubwa, hivyo ni lazima wawape viongozi muda wa kuwachuja lakini akawataka wasiwanunie baada ya kufanya uamuzi.
Rais Kikwete alisema hayo jana katika hotuba yake ya kuvunja Bunge ambayo iliibua waziwazi ushabiki kwa wagombea, hasa baada ya kumtaja aliyekuwa waziri mkuu wake wa kwanza, Edward Lowassa kwa ajili ya kumshukuru.
Akitoa salamu zake kwa wagombea hao, Rais Kikwete aliwapongeza na kuwatakia mafanikio mema katika safari yao.
“Wale wanaogombea urais waliomo humu (bungeni) nawatakia kila la kheri na nawashukuru kwa kuonyesha nia ya kunipokea mzigo huu mzito. Nawatakiwa heri katika matamanio yenu,” alisema Rais Kikwete ambaye aliingia Ikulu mwaka 2005.
“Mko wengi, wote ni vigogo na mmetupa kazi kama kamati kuwachuja kwa hiyo msitununie tukifanya maamuzi.”
Lowassa afunika
Wakati akihitimisha hotuba hiyo, Rais aliwashukuru watu mbalimbali waliofanya kazi kwenye Serikali yake, lakini hali ilikuwa tofauti alipomtaja Lowassa ambaye alifanya naye kazi kwa miaka miwili.
Alimshukuru pia, Makamu wake, Dk Mohamed Gharib Bilal, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na baadaye wabunge na viongozi wengine.
Alianza kwa kuwashukuru huku akiwataja majina. Kila alipotaja majina ya viongozi hao, wabunge walipiga makofi kwa kugonga meza zao. Hata alipomtaja Dk Bilal na Pinda, wabunge hao walishangilia kwa kawaida.
Hata hivyo, alipofikia kutaja jina la Lowassa, kelele za wabunge zilikuwa maradufu, wengi wao wakipiga meza kushangilia, hali iliyomfanya Rais Kikwete anyamaze kwa sekunde kama 50 na ndipo Lowassa aliposimama na kuinamisha kichwa kuonyesha kukubali shukrani hizo.
Wabunge waliendelea kumshangilia hadi alipoketi na ndipo Rais Kikwete akaendelea kutoa shukrani kabla ya kuhitimisha hotuba yake ya saa mbili na dakika 20.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment