Kanda ya Ziwa Wawachambua Magufuli Pamoja na Slaa Kupata Sifa za Kiongozi Bora

WAKAZI mbalimbali wa mikoa ya Kanda ya Ziwa wamewachambua wagombea urais, Dk. John Magufuli (CCM) na Dk. Willbrod Slaa (Ukawa) wakielezea wanavyowafahamu na wanachotarajia kutoka kwao ikiwa watachaguliwa kuongoza nchi.
Wengi waliohojiwa na Raia Mwema kwa nyakati tofauti wiki hii wamepongeza uteuzi wa wagombea hao wakisema wanafaa kuwa urais na wengine wamewakosoa kwa kutaja dosari zinazowapunguzia sifa za kukabidhiwa wadhifa huo.
Kabla ya kuteuliwa kupeperusha bendera ya CCM katika kinyang'anyiro hicho, Dk. Magufuli alikuwa Waziri wa Ujenzi na Dk. Slaa alikuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kilichoungana na CUF, NCCR - Mageuzi na NLD kuunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Justin Manga (38)
Kwa ujumla nimepokea kwa furaha kubwa uteuzi wa Dk. Magufuli kwa ajili ya kukiwakilisha Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika kinyang’anyiro cha urais mwaka huu.
Kwa hakika CCM wamefanya uamuzi mgumu ambao bila shaka umekidhi mahitaji ya wananchi wengi. Binafsi nilitamani kuona kama si Makongoro Nyerere wanamleta Magufuli, nafurahi kuona ndoto yangu imetimia.
Uteuzi wa Magufuli umeibua mjadala mzito, kila kona ya nchi yetu wananchi wengi wanafurahia uteuzi wake kwa sababu tunamfahamu ni mtendaji mahiri. Hakika CCM hawakufanya kosa, wamefanya uamuzi sahihi sana.
Uteuzi wa Magufuli umeua nguvu ya Dk. Slaa na Ukawa kwa ujumla. Magufuli akianza kampeni baadhi ya wapinzani na wana Ukawa watashawishika kuhamia CCM kumuunga mkono.
Dk. Benedicto Lukanima (43)
Dk. Magufuli hana ubavu wa kumshinda Dk. Slaa katika nafasi ya urais. Tutarajie kushuhudia Dk. Slaa akipata ushindi mnono katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
Unajua Dk. Slaa anakubalika kwa wananchi wengi, hasa vijana kwa sababu ni mwadilifu, hana kashfa na anao uwezo mkubwa wa kuongoza kwa hekima tofauti na Dk. Magufuli ambaye wizara aliyokuwa akiiongoza inakabiliwa na kashfa ya matumizi mabaya ya fedha.
Shaaban Itutu (37)
Mimi ni miongoni mwa Watanzania wengi wanaoamini kwamba Dk. Magufuli anatosha kwa urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu. Huo ndio ukweli usiobishaniwa.
Ninasema hivyo kwa sababu ni jambo lililo wazi kwamba Dk. Magufuli atapata kura nyingi na kumshinda kwa mbali sana Dk. Slaa wa Ukawa. Watanzania wengi wanamhitaji Dk. Magufuli kutokana na uchapa kazi wake mzuri na unaoakisi maslahi ya Taifa.
Suzana Emma (29)
Mimi sikuwa na sababu ya kuwaunga mkono CCM katika Uchaguzi Mkuu ujao kama wangefanya kosa la kumteua mgombea mwingine tofauti na Magufuli. Vivyo hivyo, sina sababu ya kuwaunga mkono Ukawa na Dk. Slaa maana ninaamini Magufuli anatosha.
Ukweli ni kwamba CCM wamesoma alama za nyakati, bila Magufuli wangeiaga Ikulu kupitia uchaguzi wa mwaka huu. Kwa sababu hiyo, namshauri babu yangu, Dk. Slaa apumzike siasa maana hawezi kumshinda Magufuli.
John Katinde (69)
Kwa maoni yangu binafsi, nadhani Dk. Slaa ana chance (nafasi) kubwa ya kuwa rais kuliko Dk. Magufuli. Kwanini ninasema hivyo?
Magufuli anaweza kuwa mtendaji mzuri lakini chombo kinachombeba (CCM) kinaweza kumnyima uhuru na nguvu ya kufanya uamuzi mgumu kwa masuala yenye maslahi ya umma.
Dk. Magufuli ni msafi ndani ya CCM na nikiri wazi kwamba chama hicho kimefanya kazi nzuri ya kukiokoa kwa kumsimamisha mgombea safi, lakini na Dk. Slaa ni mzuri kwenye Ukawa maana anauzika kwa jamii na vijana wengi wanamkubali.
Lucas Mororo (46)
Watanzania wengi tuna imani kubwa sana na Dk. Magufuli kwa sababu tumekuwa tukiona jinsi utendaji wake ulivyokuwa mzuri katika kila wizara aliyoongoza. Halafu ni mtu makini sana.
Pia Magufuli ni mtu jasiri sana, haogopi kufanya uamuzi mgumu wa papo kwa hapo. Tumekuwa tukishuhudia jinsi anavyokemea hata wakandarasi wa ujenzi wa barabara na kuwachukulia hatua kali pale wanapoonekana kuboronga kazi.
Dk. Magufuli amesababisha sasa hivi Ukawa na wapinzani kwa ujumla wameingiwa wasiwasi na baadhi yao wameanza kumuunga mkono. Kwa kifupi ni kwamba Dk. Slaa hawezi kujipima kwa Dk. Magufuli.
Tumchague Dk. Magufuli airejeshe na kuiimarisha nchi katika misingi ya uadilifu na uwajibikaji kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla.
John Mseti (40)
Tutasema mengi sana, lakini bado Dk. Slaa ana nguvu kubwa ya kisiasa nchini na anauzika kwa wananchi wengi kuliko Dk. Magufuli ambaye hata jimboni kwake (Chato mkoani Geita) baadhi ya watu hawamkubali.
Wengi tunaamini kwamba Dk. Slaa ndiye atakayeivusha nchi yetu kutoka kwenye wimbi la matumizi mabaya ya madaraka na mali za umma. Bila Dk. Slaa maisha bora kwa kila Mtanzania hayawezekani.
Lakini kwa upande mwingine, binafsi nimefurahi kuona kipindi hiki vyama vikubwa vya siasa nchini vimewateua madaktari kugombea urais. Bila shaka mpambano wa safari hii utakuwa na mvuto wa kipekee.
Mariam Masunga (70)
Ninachoweza kuamini ni kwamba Chama Cha Mapinduzi kimeponea tundu la sindano kwa sababu kila mtu alikuwa anasuburi kifanye kosa la kumteua mgombea asiyekubalika ili tuking’oe madarakani na kuwapeleka Ikulu wapinzani.
Lakini kwa kitendo cha kumleta Dk. Magufuli, njia ya ushindi ni nyeupe kwa CCM. Mwanzoni nilikuwa namuunga Dk. Slaa, ila sasa nimegeukia kwa Magufuli. Waswahili wanasema chema chajiuza, kibaya chajitembeza na mwenye macho haambiwi tazama.
CHANZO:RAIA MWEMA
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment