Askofu Gwajima: Siwezi Kuwatupa Dk Slaa, Lowassa

Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima jana alihubiri akiwa katika kiti cha magurudumu na kusema hawezi kuwatupa Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kwa kuwa ni marafiki zake wa siku nyingi.


Pia askofu huyo, amewataka waumini wote wa kanisa hilo kufika katika Kituo Kikuu cha Polisi, Alhamisi ijayo siku ambayo atakwenda kukamilisha mahojiano dhidi ya tuhuma za kumtukana Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Polycarp Kardinali Pengo.


Akihubiri mamia ya waumini waliofika kanisani hapo kwa ajili ya ibada ya Pasaka jana, Gwajima alisema kumekuwa uvumi kwamba kuhojiwa kwake na polisi kulitokana na kuwakaribisha wanasiasa hao kanisani kwake kwa nyakati tofauti na kuzungumza na waumini wake.


Alisema alifahamiana na Lowassa tangu mwaka 1996 wakati huo mbunge huyo akiwa Waziri wa Ardhi na tangu kipindi hicho amekuwa mtu wake wa karibu.


Alisema alifahamiana na Dk Slaa tangu mwaka 1994 kabla hajagombea nafasi ya urais kupitia Chadema na kwamba tangu wakati huo amekuwa rafiki wa familia.


“Hawawezi kunichagulia marafiki, hawa ni watu wangu wa karibu hata kabla hawajawa na ndoto za kugombea urais, nitaendelea kuwa nao karibu,” alisema.


Asimulia mahojiano


Akizungumzia mahojiano yake na polisi, Gwajima aliwaeleza waumini wake kwamba mambo mengi aliyohojiwa hayakuhusiana na suala la kumkashifu Kardinali Pengo.


“Polisi walinihoji mambo mengi binafsi yanayonihusu mimi na hayakuhusiana kabisa na Pengo, maswali ya Pengo yalikuwa machache sana,” alisema.


Hata hivyo, Gwajima alisema hana ugomvi na polisi wala Serikali kwa kuwa amekuwa akitoa ushirikiano kwa vyombo hivyo. Akitoa mfano, alisema Februari mwaka huu alipeleka barua polisi kueleza anataka kudhamini kampeni kwa ajili ya kupinga mauaji ya albino kwa kushirikiana na jeshi hilo.


“Niliwaeleza kwamba tungezunguka na polisi mikoa yote Tanzania na wamenijibu kwamba nipeleke ratiba ya shughuli hiyo ili tuanze,” alisema.


Alisema pia alidhamini mafunzo ya ulinzi shirikishi kwa vijana 400 kwa kushirikiana na polisi... “Shughuli hizi zinaonyesha kwamba sina ugomvi na polisi, bali nimekuwa rafiki kwa kushiriki katika shughuli zenye masilahi kwa Taifa.”
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment