ACT Kuchukua Majimbo Manne ya Uchaguzi Mkuu Mwaka Huu

Chama cha Alliance for Change and Transparency (ACT), kimesema kinatarajia kunyakuwa majimbo manne ya ubunge katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba, mwaka huu.
Kimetaja majimbo hayo kuwa ni Ubungo, ambalo linaongozwa na John Mnyika (Chadema), Kawe linaloshikiliwa na Halima Mdee (Chadema), Segerea ambalo Mbunge wake ni Makongoro Mahanga (CCM) na Kahama la James Lembeli (CCM).
Kiongozi Mkuu wa Chama hicho, Zitto Kabwe, alisema hayo katika kipindi cha Hot Mix kinachorushwa na kituo cha EATV.
Zitto aliendeleza msimamo wake wa kutogombea ubunge kwenye jimbo lake la awali la Kigoma Kaskazini.
"Nina maombi jimbo la Kahama, Kawe, Ubungo na Segerea lakini kwa kuwa ACT kinaongozwa kizalendo, tutaweka utaratibu mzuri wa kuweka wagombea kila eneo, binafsi kwa sasa siwezi kusema wapi nitagombea," alisema.
Alipoulizwa ni eneo gani kati ya hayo aliyoyataja huduma yake inahitajika, alijibu kwa kifupi kuwa, nchi nzima ina muhitaji.
"Kabla ya kampeni kuanza wagombea wakirudisha fomu ndipo mtajua Zitto anagombea jimbo gani, lakini lazima niongozwe na chama nikagombee wapi , wanaweza kusema Zitto kagombee jimbo A," alisema.
Aliongeza kuwa, ACT kinahitaji kujipanga kuingia kwenye mapambano ya kufyeka msitu wa siasa kwa kuwa ndani yake kuna vyama zaidi 22 na vingine vikiwa na uzoefu mkubwa kutokana na kudumu zaidi ya miaka 23.
Alisema kazi kubwa walionayo ni kukijenga chama ili kiweze kulirudisha taifa kwenye misingi ya waasisi waliyoiacha.
Aliongeza kuwa, baadhi ya watu wanamuona kama anaanza upya kwa sababu wapo wachache waliwahi kujaribu na kuishia njiani.
Alipoulizwa kuhusu wachambuzi wa siasa wanavyomchukulia hivi sasa, Zitto alisema wapo wenye mtazamo hasi na wengine chanya.
Alisema kwa wale wanaomchukulia kwa mtazamo hasi anaendelea kuwafundisha na kuwaonyesha kwamba muono wao ni tofauti wakati wale wa chanya anaendelea kuwasikiliza ili kupata muongozo zaidi kutoka kwao.
"Tukumbuke hii nchi watu wamezoea kuchukia mabadiliko angalia kwenye sanaa wakimuona Diamond amefanikiwa waanza kutoa maneno ambayo siyo, watu wanachukia mabadiliko," alisema.
Kuhusu kuitwa msaliti ndani ya Chadema kwa madai kuwa baada ya kuikosesha Chadema jimbo kule Katavi, alisema jambo hilo siyo la kweli na kwamba amekitumikia chama hicho nusu ya maisha yake na alichokifanya kinafahamika kwa wanachama na viongozi.
"Ambacho sikufanya mimi ni binadamu sipo sawa kwa kila kitu hakuna binadamu ambaye hana makosa lakini yapo mema ambayo nimefanya lakini sasa nimeyakunja na kuyaweka pembeni na tumechora mstari na kuanzisha chama cha siasa cha wazalendo," alisema.
Kuhusu kurasa zake kwenye mitandao ya kijaamii kuwa na maoni hasi, Zitto alisema kila mtu ana mawazo yake na hawezi kuyabadisha.
"Wito wangu ni kwa watu ambao ni waoga wa kuchukua maamuzi, waweke akiba ya maneno kwa sababu ACT ni sawa na moto wa pumba ambao ukiwaka juu unadhani hakuna moto lakini ukiweka mguu kuna moto mkali sana," alisema
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment