Ukawa Wavuruga Bunge Dodoma

Wabunge wa upinzani wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) jana walianzisha tafrani bungeni na kusababisha kikao cha Bunge kuvunjika saa 5.18 asubuhi baada ya kusimama na kupaza sauti wakishinikiza Serikali itoe kauli juu ya hatima ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura na upigaji wa Kura ya Maoni kupitisha Katiba Inayopendekezwa.
Huku wakiwa wamesimama walikuwa wanapiga kelele wakisema, ‘hatutaki kuburuzwa’, ‘tumechoka kupelekeshwa’, Watanzania wapo njia panda’ na ‘tunataka majibu,’ ‘Bunge lisitumiwe kuilinda Serikali’, ‘Waziri Mkuu yupo bungeni kwa nini asitoe kauli’ na maneno mengine mengi bila mpangilio.
Wabunge hao wa vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema na CUF, kwa umoja wao walimtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kutoa majibu hayo muda huohuo, kabla ya jioni kutoa hutuba na kuahirisha mkutano huo wa 19 wa Bunge.
Baadaye jana usiku katika hotuba yake ya kuahirisha Bunge hadi Mei 12, utakapoanza Mkutano wa 20, Waziri Mkuu Pinda alisema Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) itatoa taarifa siku za hivi karibuni kuhusu upigaji wa kura ya maoni.
“Ni dhahiri muda uliobaki kuanzia sasa ni mfupi lakini Tume ndiyo itakayotujulisha ratiba kamili,” alisema.
Sakata lilivyoanza
Kelele hizo zilitokana na hoja za wabunge wawili, Suleiman Jafo wa Kisarawe na yule wa Ubungo, John Mnyika waliotaka Bunge lisitishe shughuli zake zote lijadili suala hilo kwa kuwa ni muhimu na Taifa halielewi hatima yake, wakati Bunge lilikuwa linaahirishwa jana.
Spika wa Bunge, Anne Makinda alikataa suala hilo kujadiliwa, akisema ni hoja iliyowasilishwa katika mkutano uliopita, akataka Bunge liendelee na shughuli zake, lakini wabunge wa upinzani walikataa kukaa na wakaendelea kupaza sauti.
Hata alipobadili kauli akasema, “nimesema kauli itatolewa, wabunge hao walisisitiza itolewe papohapo. Hata alipowataka waondoke ndani ya ukumbi huo, wabunge hao ambao ni wachache ukilinganisha na wale wa CCM, walikataa, wakisema; “hatutoki hadi kauli itolewe.”
Kelele za wabunge hao zilimfanya Spika Makinda kutoa kauli kali, “Njooni mwendeshe (kikao) nyinyi basi. Njooni hapa mkae tena wote.”
Baada ya kuona kelele hizo zimedumu kwa dakika tatu, Spika Makinda alilazimika kusitisha shughuli za Bunge hadi baadaye (jioni), bila kutaja muda ambao Bunge lingerejea na kuwaacha wabunge wakiwa wamesimama katika makundi ndani ya ukumbi wakijadili tukio hilo.
Jafo ndiye aliyeanza kuomba mwongozo wa Spika akitaka chombo hicho cha kutunga sheria kisitishe kujadili jambo lolote lile, badala yake kijadili mustakabali wa Katiba Mpya, akitaka Serikali iwasilishe muswada wa sheria kwenye mkutano wa 20 wa Bunge (wa Bajeti) ili Katiba ya Mpito ipitishwe.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment