Ngeleja Azima Hoja ya Escrow

MBUNGE wa Sengerema, mkoani Mwanza, Bw. William Ngeleja, amesema wapinzani wake kisiasa wanapoteza muda wao wanapotoa hoja dhaifu kwa wananchi wa jimbo hilo juu ya kuhusika kwake kwenye sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow na kuzungumzia tatizo la maji.

Bw. Ngeleja aliyasema hayo juzi kwenye mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Pambalu,
Kata ya Ibisabageni, wilayani humo akiwa katika mwendelezo wa ziara zake za kukagua na kusimamia miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa jimboni humo.

"Baadhi ya wapinzani wangu kisiasa wanatumia hoja dhaifu ambazo hazina mashiko ikiwemo ya sakata la Escrow na tatizo la maji kutaka kunimaliza...leo nimekuja hapa kuwaambia ukweli juu ya mambo hayo ili ukweli ujulikane.

"Mwaka 2014, tulikuwa na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji, hapa Sengerema CCM ilishinda kwa asilimia 83 na wapinzani wetu CHADEMA waliambulia asilimia 17, najua tungeweza kupata ushindi zaidi ya huo lakini nchi ilitikiswa na masuala mawili likiwemo la Escrow na Katiba Mpya," alisema.

Aliongeza kuwa, katika sakata la Escrow, watu wasifikiri kuna ujanja wowote ulifanyika; bali fedha alizopewa ni msaada kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo jimboni kwake, uchangiaji harambee kwenye makanisa, misikiti na vikundi vya ujasiriamali.

Alisema msaada huo umetoka kwa wafadhili ili kusaidia wananchi; hivyo si kosa wala dhambi kupokea msaada kwani ruzuku inayotolewa na Serikali pekee, haitoshi kumaliza kero mbalimbali za wananchi hususan jimboni humo.
"Leo (jana), nimekuja na orodha ndefu inayoonesha jinsi nilivyotumia sh. milioni 40 nilizopewa kama msaada ambazo pia nilizilipia kodi kwa mujibu wa sheria na fedha zilizobaki, zilikuwa sh. milioni 27 pekee.

"Dhamira yangu ilikuwa kuwasaidia wananchi wangu, lakini bado taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), hakuna sehemu inayonitaja, suala hili lililetwa bungeni kupitia Kamati ya Bw. Zitto Kabwe (Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali-PAC)," alisema.

Bw. Ngeleja alifafanua kuwa, Bw. Kabwe ni miongoni mwa watu waliopokea mgawo kutoka kwa mmiliki wa Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited, James Rugemalira ambaye alimpa sh. milioni 33 lakini yeye hakujadiliwa licha ya kutolewa vielelezo vyote bungeni.

"Kutokana na jambo hili, ukiliangalia kwa makini utagundua kuwa, wengine wakipewa misaada hakuna shida, lakini akipewa Ngeleja ni nongwa," alihoji Bw. Ngeleja.

Akizungumzia tatizo la maji linalowakabili wananchi jimboni humo, Bw. Ngeleja alisema hicho ndicho kipaumbele chake kikubwa akiwataka wananchi wawe watulivu kwani muda si mrefu, tatizo hilo litakwisha na kubaki historia.

"Upatikanaji wa maji katika maeneo mengi nchini ni tatizo la kitaifa, kero hii katika jimbo langu naifahamu na wananchi wa jimbo langu pia ni mashahidi, hivi sasa kuna mradi mkubwa wa maji ulioanza kutekelezwa wenye thamani ya sh. bilioni 23; hivyo wanaotumia kero hii kutaka umaarufu watakosa la kusema baada ya kukamilika," alisema.

Bw. Ngeleja ambaye amewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, mradi huo unatakiwa kukamilika Januari 2016 lakini kutokana na ukubwa wa tatizo hilo, wamekubaliana na
Mkandarasi atandaze bomba kubwa la maji kutoka Nyamazugo ili huduma hiyo ipatikane mapema.

Katika mkutano huo, Bw. Ngeleja alitoa fursa kwa wananchi waulize maswali ambao wengi wao walitaka kujua ukweli juu ya kuhusika kwake kwenye sakata la Escrow na tatizo la maji lakini waliridhika na majibu aliyowapa.

Miongoni mwa wananchi waliouliza maswali, Bw. James John, alitaka kufahamu kama Bw. Ngeleja alihusika katika kashfa hiyo, wengine wakitaka kujua hatua anazochukua
kukabiliana na tatizo la maji, mrundikano wa mahabusu katika Gereza la Wilaya Kasungamile.

Mambo mengine waliyotaka majibu ya Bw. Ngeleja na tatizo la ajira kwa vijana ambapo mama mmoja anayeitwa Letisia William, alimtaka mbunge huyo kupeleka hoja binafsi bungeni ili kuzuia unywaji pombe aina ya viroba kwa vijana.

Baada ya Bw. Ngeleja kumaliza mkutano huo, wananchi walimsindikiza kwa maandamano kwenda Ofisi za CCM wilayani humo wakicheza nyimbo za aliyekuwa kada
wa chama hicho marehemu John Komba.

Kwa upande wake, Meneja wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira wilayani humo, Bw. Wawa Nyonyori, aliwahakikishia wananchi jimboni humo kuwa mradi huo utakamilika kama ulivyopangwa.

"Yametengenezwa matangi matano kwa ajili ya kuhifadhi maji yanayotokana na mradi huo," alisema.

Naye Mkandarasi Mshauri wa Kampuni ya China Civil Engineering, Bw. Marco Nyagabona, alisema wameweka kipaumbele katika mradi huo ili ukamilike kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Bw. Ngeleja alivunja mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), katika Kijiji cha Ibondo, wilayani humo baada ya wananchi kuukimbia na kuhudhuria mkutano wake.

Mkutano huo ulikuwa ufanyike katika Uwanja wa Shule ya Msingi Ibondo, ukiongozwa na Diwani wa Kata ya Nyampulukano, Bw. Emmanuel Mnwanis, umbali wa mita 50 kutoka eneo ambalo Bw. Ngeleja alikuwa akifanya mkutano wake.

CHADEMA walitumia mbinu mbalimbali zikiwemo matangazo na muziki ili kuwavuta wananchi, lakini hali haikuwa shwari kwani wananchi waliendelea kumsikiliza Bw. Ngeleja na kusababisha mkutano huo usifanyike.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment