ATCL Yazindua Ndege Nyingine Mpya Aina ya CRJ - 100


Abiria wakishuka toka kwenye ndege mpya ya Shirika la Ndege la Taifa, Air Tanzania (ATCL) aina ya CRJ-100 yenye uwezo wa kubeba abiria 50 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki wakitoa mkoani Kigoma. Huo ukiwa ni mkakati wa kimaendeleo wa shirika hilo katika kuongeza idadi ya ndege na safari zake.
Meneja wa Air Tanzania (ATCL) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa 
Julius Nyerere, Bw James Mbago akizungumza na waandishi wakati wa 
uzinduzi wa ndege mpya ya shirika hilo aina ya CRJ-100 yenye uwezo wa 
kubeba abiria 50, mara baada ya ndege hiyo kutua ikitokea mkoani Kigoma.
Huo ukiwa ni mkakati wa kimaendeleo wa shirika hilo katika kuongeza 
idadi ya ndege na safari zake. 
SHIRIKA la ndege la Taifa (ATCL) mwishoni mwa wiki iliyopita lilizindua ndege yake mpya aina ya CRJ-100 yenye uwezo wa kubeba abiria 50 ikiwa ni sehemu ya mpango wa shirika hilo kuongeza idadi ya ndege zake sambamba na kuongeza idadi ya safari zake.

Shirika hilo ambalo kwa sasa linalotoa huduma zake katika mikoa ya Dar es Salaam, Kigoma, Mtwara na visiwa vya Komoro limejipanga kufanya safari za kila siku kati ya mikoa ya Dar es Salaam na Kigoma huku pia likiwa tayari kufanya safari za Mtwara na visiwa vya Komoro mara sita kwa wiki katika siku za Jumatatu, Alhamisi na Jumamosi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam  mara tu baada ya ndege hiyo kutua kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Meneja wa shirika hilo katika kiwanja hicho,  James Mbago alisema ndege hiyo imekodiwa kutoka nchini Afrika Kusini kwa jitihada za Serikali ya Tanzania na sasa ipo tayari kuwahudumia wateja  wa shirika hilo.

“Kuja kwa ndege hii kunaongeza idadi ya ndege zetu hadi  kufikia mbili na tunashukuru kuona kwamba imepokelewa vizuri na abiria  wetu. Ndege yetu nyingine aina ya De-Havilland Dash 8 Q300 kwa sasa  inapata matengenezo makubwa kwenye karakana yetu iliyopo hapa hapa  uwanja wa ndege,’’ alisema Mbago.

Kwa mujibu wa Mbago kupona kwa ndege hiyo inayofanyiwa matengenezo kiwanjani hapo kutalifanya shirika hilo lianzishe tena  safari zake za ndani kwa mikoa ya Mwanza, Tabora, Arusha na Mbeya.

“Muda si mrefu mambo yatakuwa mazuri zaidi…inafurahisha zaidi tunapopata mrejesho mzuri kutoka kwa wateja wetu wanaofurahia huduma za shirika lao mama,’’ aliongeza Mbago. Zaidi, Mbago aliongeza kuwa shirika lake linatarajia ongezeko kubwa la abiria kutokana na ukweli kuwa ndege yao hiyo mpya inauwezo wa kusafiri kwa haraka zaidi ikilinganishwa na ndege nyingine huku safari zake zikiambatana na huduma nzuri inayotolewa kwa wateja wake.

Wakizungumza mara tu baada ya kushuka kwenye ndege hiyo, baadhi ya abiria waliotoka Kigoma walisema licha ya kutumia muda mfupi zaidi lakini pia walifurahia huduma nzuri walizozipata kutoka kwa wahudumu wa ndege hiyo.



“Kwa kweli hii ilikuwa ni moja ya safari zangu za ndege ambayo nimeifurahia sana. ATCL wanahitaji pongezi kwenye hili na zaidi wafikirie kuboresha huduma zaidi ya hapa…sisi abiria tupo tayari kuwaunga mkono kwa sababu ndio wanabeba nembo ya taifa letu,’’ alisema mmoja wa abiria hao aliyejitambulisha kwa majina Gaudence Kashoka.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment