JK: Maaskofu Walitoa Matamko ya Hasira

Wakati Rais Jakaya Kikwete akisema msimamo wa Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF) wa kuwataka waumini wao kuipigia kura ya hapana Katiba Inayopendekezwa ni wa hasira pia usiokuwa na tija kwa maendeleo ya Taifa, baadhi ya maaskofu wameshikilia msimamo huo.
Rais Kikwete alitoa kauli hiyo jana katika mkutano wa kamati ya amani ya Mkoa wa Dar es Salaam iliyoshirikisha wajumbe kutoka mikoa mbalimbali nchini unaowajumuisha viongozi wa dini za Kiislamu na Kikristo akilenga kuzungumzia tamko hilo la TCF walilolitoa Machi 12, mwaka huu.
Katika tamko hilo lililosainiwa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Askofu Dk Alex Malasusa, Mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa na mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania (CPCT), Askofu Daniel Awet liliwataka waumini wake kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura na kuipigia kura ya hapana Katiba hiyo.
Jukwaa hilo lilitaja sababu mbili za uamuzi wake huo kuwa ni Muswada wa Mahakama ya Kadhi kukiuka misingi ya Taifa kuwa na Serikali isiyo na dini na Kura ya Maoni kusababisha mgawanyiko.
“Hivyo basi, Jukwaa linawataka waumini wake wote wajitokeze kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, waisome Katiba Inayopendekezwa na kushiriki kikamilifu vipindi vya elimu juu ya Katiba Inayopendekezwa na kisha wajitokeze kwa wingi kupiga kura ya hapana,” lilisema tamko hilo.
Katika hotuba yake iliyodumu kwa saa 1.16, Rais Kikwete alianza kwa kuwaomba radhi viongozi hao kwa kuchelewa kwa akisema alikuwa na majukumu mengi. Mkutano huo ulikuwa uanze saa 3.00 asubuhi lakini Rais Kikwete alifika saa 6.30 mchana.
Alisema “Taifa linapitia hali isiyokuwa ya kawaida, tusipokuwa makini kuidhibiti itakuwa ni tatizo, ni kazi kubwa inayohitaji moyo, uvumilivu na viongozi wenye kujali masilahi ya Taifa.”
“Mwelekeo wa mambo hauhitaji uwe bingwa kujua hali hairidhishi sana na kama hatutachukua hatua hatuwezi kufika na tutasababisha uvunjifu wa amani za kidini na moto wake ni mkali sana,” aliongeza Rais Kikwete aliyekuwa akizungumza kwa umakini na taratibu.
Jukwaa la wakristo
Kuhusu tamko la Jukwaa la Wakristo, Rais Kikwete alisema wakati Taifa likisubiri kuona mchakato wa Katiba unakwenda hatua za mwisho kumekuwapo na matamko kadhaa ambayo hayakumfurahisha.
“Nimeyasoma matamko hayo yote kwa umakini, imenishangaza, imenisikitisha na kunihuzunisha. Siamini kwa nini wamefikia huko kwa kuunga au kutokuunga mkono,” alisema Rais Kikwete aliyekuwa akizungumza kwa sauti ya chini wakati wote wa hotuba yake.
“Kinachonisumbua ni kuipa sura na mtazamo wa kidini Katiba Inayopendekezwa, kama ingekuwa inakinzana na uhuru wa kuabudu hapo ingekuwa sawa lakini ibara ya 41 inatambua uhuru wa kuabudu na kuitangaza dini, sasa katika mazingira hayo kuwaeleza waumini kuikataa inanipa tabu sana,” aliongeza.
Credit: Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment