Nyalandu: Urais CCM, Ukawa ni Kivumbi

Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu amesema uchaguzi wa Rais ajaye utakuwa na ushindani mkubwa ndani na nje ya CCM, huku akibainisha kuwa haogopi mtu kati ya wote wanaotajwa kwenye kinyang’anyiro hicho, bali anawaheshimu.
Lakini mbunge huyo wa Singida Kaskazini amesema mgombea pekee atakayemwogopa ni yule atakayekuwa anataka kulipiza kisasi dhidi ya wagombea wengine.
Waziri huyo alitoa kauli hiyo jana wakati alipofanya ziara kwenye makao makuu ya Ofisi za Mwananchi Communications inayozalisha magazeti ya The Citizen, Mwananchi na Mwanaspoti zilizoko Tabata Relini kando ya Barabara ya Mandela.
“Sipendi kulizungumzia sana jambo hilo,” alisema Waziri Nyalandu ambaye huzungumza kwa sauti ya chini na taratibu... “Kwenye chama chetu (CCM) muda wake bado. Lakini naweza kusema kuwa mwaka huu ni wa ushindani mkubwa ndani ya CCM na ‘opposition’,” aliwaambia wahariri wa Mwananchi Communications.
“Mwisho tutakuwa na kambi ya CCM. Kwaya ya CCM itapambana na kwaya nyingine ambayo ina sauti zote nne kama CCM,” alisema akimaanisha kuwa upinzani nao utakuwa umekamilika na kusisitiza muda ukifika atachukua fomu.
Kauli ya Nyalandu imekuja wakati nchi ikijiandaa kuingia kwenye Uchaguzi Mkuu utakaoiweka madarakani Serikali ya Awamu ya Tano, hali ambayo inaipa shida CCM kumpata mrithi wa Rais Jakaya Kikwete ambaye pia atalazimika kuachia uenyekiti wa chama hicho.
Tayari wanachama wanne wa CCM wameshatangaza nia, akiwamo Nyalandu. Wengine ni Hamisi Kigwangala, ambaye ni Mbunge wa Nzega, January Makamba (Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia) na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
Hata hivyo, kinyang’anyiro kikubwa kinatarajiwa kuwa miongoni mwa makada wa muda mrefu wakiongozwa na Edward Lowassa, ambaye alikuwa Waziri Mkuu na Bernard Membe (Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), ambao hawajatangaza nia, lakini wanatumikia adhabu ya kufungiwa kwa zaidi ya miezi 12 kwa makosa ya kukiuka taratibu za chama hicho kwa kuanza kampeni mapema.
Wengine wanaotajwa kwenye mbio hizo ni Mwigulu Nchemba, ambaye ni Naibu Waziri wa Fedha (Sera), Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasira, Mbunge wa Songea Mjini, Emmanuel Nchimbi, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.
Wakati CCM ikiwa na kazi ya kumpata mgombea wake wa urais, hali ni ngumu zaidi safari hii nje ya chama hicho kutokana na vyama vinne vya upinzani kukubaliana kusimamisha mgombea mmoja kwenye kila nafasi.
Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD vimeunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na vimesaini makubaliano ya kusimamisha mgombea mmoja.
Nyalandu, ambaye alitangaza nia yake wakati akiwa jimboni kwake, alisema mjadala wa kuelekea Uchaguzi Mkuu unatakiwa ujikite kwenye masuala ya kuiondoa nchi kutoka hapa ilipo na kwenda juu zaidi.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment